Serikali kuendelea kuenzi utamaduni wa Mtanzania

0
204

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Abdallah Ulega amesema kuwa, Serikali itaendelea kuenzi na kulinda utamaduni wa Mtanzania kwa manufaa ya vizazi vilivyopo na vijavyo.

Naibu Waziri Ulega ametoa kauli hiyo mkoani Kigoma wakati akizungumza na wadau wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa mkoa huo.

Amewaagiza maafisa utamaduni katika mikoa yote nchini kuhakikisha kwenye maeneo yao wanatenga maeneo maalumu ambayo yataonesha na kuelezea utamaduni wa wakazi wa eneo husika.

Naibu Waziri huyo wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesisitiza malezi ya watoto yazingatie kuwarithisha utamaduni wa Mtanzania kwa sababu utamaduni ni utajiri na ndio maana duniani kwa sasa kuna utamaduni wa utalii.