Yanga waleee kileleni, Azam yatoboa kwa Mbeya City

1
1106

Katika muendelezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara, timu za Azam na Yanga zimepata ushindi na kuondoka na alama tatu katika michezo miwili tofauti iliyopigwa leo.

Mapema katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya wanalambalamba kutoka Chamazi, Dar es Salaam waliwaadhibu vijana wa Mbeya City kwa bao moja bila, goli likifungwa na Idris Mbombo na kuwafanya azam kufikisha alama nane baada ya kucheza michezo minne.

Nao Wananchi wenye maskani yao mtaa wa Jangwani Kariakoo jijini Dar es Salaam, wametoa kichapo kitakatifu kwa walima miwa kutoka Manungu Turiani mkoani Morogoro Mtibwa Sugar, baada ya kuwafunga goli tatu bila magoli yakifungwa na Djuma Shabaan, Fiston Mayele na Stephan Aziz Ki.

Kwa matokeo hayo Yanga wanafikisha alama kumi na kukaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku ligi hiyo ikiendelea kesho ambapo mechi inayosubiriwa kwa hamu ni Wekundu wa Msimbazi watakapokaribishwa na wajelajela kutoka Mbeya Tanzania Prisons, katika dimba la Sokoine jijini humo.

1 COMMENT

Comments are closed.