Yanga Vs Simba Oktoba 23

0
337

Bodi ya ligi imetangaza ratiba ya msimu mpya wa michuano ya Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara, ambapo michezo 240 inatarajiwa kupigwa katika msimu wa ligi wa mwaka 2022/2023.

Akitangaza ratiba hiyo Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Almas Kasongo amesema, ligi hiyo itaanza kutimua vumbi tarehe 15 mwezi huu na itafikia tamati Mei 27 mwaka 2023.

Ratiba hiyo inaonesha pia miamba ya soka hapa nchini Yanga na Simba itavaana katika raundi ya 8 itakayopigwa Oktoba 23, 2022 saa 11 jioni katika dimba la Mkapa mkoani Dar es Salaam.

Mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo utapigwa Agosti 15 mpaka Agosti 17 mwaka huu, ambapo mabingwa watetezi wa ligi hiyo Yanga itaanzia ligi hiyo ugenini mkoani Kilimanjaro kuwavaa Polisi Tanzania, huku Simba wakianzia nyumbani Dar es Salaam kuwaalika wachimba dhahabu wa Geita.