TFF kufunga taa viwanja vyote vinavyotumika Ligi Kuu Tanzania Bara

0
286

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limeingia makubaliano na Azam Media kwa ajili ya kuboresha viwanja vinavyotumiwa na timu zinazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara.

Kwa kuanzia viwanja vitakavyofanyiwa maboresho ni viwanja vya Kaitaba (Kagera), Gwambina (Mwanza), Namungo(Lindi)na Mkwakwani (Tanga).

Miongoni mwa maboresho yatakayofanywa kwenye viwanja hivyo ni pamoja na kufungwa taa ili kuwezesha michezo mingi zaidi kuchezwa nyakati za usiku na kuachana na michezo ya saa nane mchana.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, maafisa wa TFF na muwakilishi wa Azam Media wameeleza kuwa endapo uwanja uliofanyiwa maboresho utaonekana hautumiki kwa sababu yoyote ile ikiwa ni pamoja na timu kushuka daraja, vifaa vilivyofungwa vinaweza kuondolewa.

Maboresho hayo yatafanyika kwa awamu ambapo wamesema hadi mwaka 2025 wanataka viwanja vyote vinavyotumika viwe na taa.