Sharapova na Federer waondolewa US Open

0
2076

Nguli wawili wa mchezo wa Tenisi Maria Sharapova na Roger Federer usiku wa kuamkia Septemba Nne mwaka huu wameondoshwa kwenye mashindano ya US Open baada ya kupoteza michezo yao ya hatua ya Kumi na Sita bora.

Roger Federer alifungwa na John Millman wa Australia ambaye yupo nafasi ya 55 kwenye ubora kwa upande wa wanaume.

Millman alitumia saa tatu na dakika 35 kumtandika nguli huyo wa Tenis,-Roger Federer baada ya kumfunga kwa Seti tatu kwa moja kwenye mchezo huo wa hatua ya kumi na Sita bora.
Baada ya kumtoa nguli Roger Federer, sasa Millman atapambana na nguli mwingine ambaye ni bingwa mara mbili wa mashindano hayo ya US Open,- Novak Djokovic ambaye amemtoa Joao Sousa wa Ureno kwenye hatua ya kumi na sita bora.

Kwa upande wa akina dada, nguli Maria Sharapova naye ameaga mashindano hayo ya US Open ya mwaka 2018 baada ya kukubali kipigo cha seti mbili kwa bila toka kwa Carla Suarez Navarro kwenye hatua ya kumi na sita bora.

Bingwa huyo mara tatu wa mataji makubwa ya Tenis (Gland Slam), – Maria Sharapova alipoteza mara tatu kwenye seti ya kwanza ya mchezo huo na kumfanya apoteza kabisa muelekeo kweye mchezo huo.

Sharapova ambaye kwa sasa ni wa 22 kwenye ubora kwa upande wa akina dada bado hajawa kwenye kiwango bora tangu arejee toka kwenye adhabu ya kutumia dawa zilizopigwa marufuku michezoni na hajawahi kuvuka hatua ya robo fainali kwenye mashindano yeyote yale kwa kipindi cha miezi 15.

Baada ya kumtoa Maria Sharapova, sasa Carla Suarez Navarro atapambana na mshindi wa pili wa mwaka 2017 kwenye mashindano hayo Madison Keys kwenye hatua ya robo fainali.