Shaffih Dauda na mwenzake walipa faini kuepuka kifungo jela

0
1555

Mwandishi wa habari Shaffih Dauda na mwenzake Benedict Felix ambaye ni mtaalamu wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), wamelipa faini ya shilingi milioni tano kila mmoja na hivyo kuepuka kifungo cha miezi 12 jela kila mmoja.

Awali mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, iliwahukumu wawili hao kulipa faini hiyo ama kwenda kutumika kifungo hicho jela, baada ya kukiri kutenda kosa la kuchapisha maudhui mtandaoni kupitia Televisheni ya mtandaoni inayomilikiwa na Shaffih Dauda bila kibali cha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisitu, Godfrey Isaya.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, washitakiwa hao walitenda kosa hilo kati ya Juni 11 na Septemba mwaka 2019 jijini Dar es Salaam, wakati wakijua kufanya hivyo ni kosa la kisheria.