Shabiki wa Spurs mbaroni kwa ubaguzi

0
1639

Shabiki mmoja wa Tottenham Hotspurs ametiwa mbaroni kwa kitendo cha kumrushia ganda la ndizi mshambuliaji wa Arsenal, -Pierre-Emerick Aubameyang wakati akishangilia bao la kwanza kwenye mchezo uliowakautanisha mahasimu hao wa Kaskazini mwa jiji la London.

Picha kutoka kwenye dimba la Emirates zinaonesha ganda la ndizi likiwa kwenye uwanja,  eneo alilosimama Aubameyang baada ya mshambuliaji huyo kwenda kushangilia bao lake la mkwaju wa penati katika dakika ya kumi mbele ya mashabiki wa Spurs.

Chama cha Soka cha England (FA) kimesema kuwa kinachunguza tukio hilo hata kama halikujumuishwa kwenye ripoti ya mwamuzi wa mchezo huo Mike Dean na polisi wa Metropolitan wamesema kuwa walimkamata shabiki huyo usiku wa Disemba pili kwa kufanya kitendo hicho ambacho hakikuabliki.

Kwa upande wao Spurs kupitia kwa msemaji wao wamesema kuwa kitendo alichofanya shabiki huyo kamwe hakikubaliki,  hivyo watamfungia shabiki huyo kutokana na vitendo hivyo vya kibaguzi na kwamba klabu hiyo haitamvumilia shabiki yoyote atakayefanya vitendo visivyokubalika kwenya mchezo wa soka.

Wakati huo huo mashabiki wengine sita wametiwa mbaroni wakiwemo wawili wa Arsenal,  kwa kosa la kuwasha miale ya moto iliyoambatana na moshi mzito baada ya timu yao kutoka nyuma kwa mabao mawili na kuibuka na ushindi wa mabao manne kwa mawili.