Samatta dimbani jumapili hii

0
494

Kivumbi cha Ligi Kuu ya England kinaendelea leo kwa mchezo mmoja kuchezwa, ambapo Wolves watakuwa nyumbani kuwakaribisha Leicester City.

Kocha wa Leicester, Brendan Rodgers anasema kiungo mkabaji Wilfred Ndidi huenda asiwe sehemu ya kikosi chake kutokana na upasuaji wa goti aliofanyiwa katika siku za hivi karibuni, huku Ryan Bennett akikosekana kutokana na vipengele vya mkataba wake wa mkopo akitokea Wolves.

Kwa upande wa Wolves, wanaimani mshambuliaji wao mweye nguvu nyingi Adama Traore atakuwa sehemu ya kikosi cha usiku wa leo licha ya maumivu ya bega aliyoyapata katika mchezo dhidi ya Manchester United, lakini watamkosa Ruben Vinagre anayesumbuliwa na tatizo la misuli.

Endapo Wolves watashinda mchezo wa leo dhidi ya Leicester, watapanda hadi nafasi ya sita ambayo wataikalia hadi jumapili kwa kufikisha alama 38 na kuishusha Tottenham Hotspur yenye alama 37.

Kesho itachezwa michezo miwili ambapo wateule Southampton watamenyana na Burnley kwenye dimba la St Marry’s huku Norwich City wakiwakaribisha vinara Liverpool.

Jumapili pia itachezwa michezo miwili ambapo Mtanzania Mbwana Samatta ataiongoza Aston Villa kumenyana na Tottenham Hotspurs dimbani Villa Park na washika bunduki wa London, Arsenal watawakaribisha Newcastle United kwenye dimba la Emirates.