Liverpool yapaa kieleleni Ligi ya England

0
1085

Liverpool imezidi kujikita kileleni mwa Ligi Kuu ya England na kuiacha Manchester City kwa alama 11 baada ushindi wa magoli manne kwa bila dhidi ya Newcastale United katika mchezo uliopigwa kwenye Dimba la Anfield.

Katika mchezo huo magoli ya Liverpool yamefungwa na wachezaji Dejan Lovren dakika ya 11 huku mchezaji Mohamed Salah akifunga kwa mkwaju wa penati dakika ya 48 na magoli mengine mawili yamefungwa na wachezaji Shaqiri na Fabinho.

Kutokana na ushindi huo Liverpool imefikisha alama 51 huku Manchester City ambao walikuwa wanaongoza ligi kwa muda mrefu wakiporomoka hadi nafasi ya tatu kwa kufikisha alama 44 baada ya kupoteza mchezo dhidi ya Leicester City  kwa kutandikiwa magoli mawili kwa moja ugenini.

Huu ni mchezo wa pili mfululizo kwa Manchester City kupoteza baada ya hivi karibuni kufungwa na Cystal Palace magoli matatu kwa mawili.

Katika mchezo huo mchezaji Ricardo Pereira ndiye alipeleka kilio Manchester City kwa kufunga goli dakika za lala salama za mchezo.

Manchester City walikuwa wa kwanza kupata goli dakika ya 14 kupitia kwa mchezaji Benardo Silva.

Leicester City wakasawazisha dakika 19 ya mchezo kupitia kwa mchezaji wake Marc Albrighton.

Nayo Tottenham Hotspur wamepanda hadi nafasi ya pili kwa kufikisha alama 45 baada ya kuichapa Bournemouth magoli matano kwa bila.

Magoli ya Tottenham yamefungwa na wachezaji Eriksen akifunga dakika ya 16, Son Heung Min akifunga magoli mawili dakika ya 23 na 70 na magoli mengine yakipachikwa na wachezaji Lucas Moura na Harry Kane.