Kocha wa Manchester United asema wataongeza bidii kupata ushindi zaidi

0
1330

Kocha wa muda wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer amesema hatajikita zaidi kwenye soka la kushambulia baada ya kikosi chake kufunga goli la 12 kwenye mchezo wa tatu akiwa kama kocha wa Manchester United wakiilaza FC Bournemouth mabao manne kwa moja.

Solskjaer anasema kila mmoja anadhani kuwa anapendelea soka la kushambulia zaidi muda wote lakini msingi wa yote hayo ni namna unavyojilinda na kutoruhusu kufungwa huku ukitengeza nafasi ya kushinda.

Decemba 30 Manchester United imeibuka na ushindi wa mabao manne kwa moja dhidi ya FC Bournamouth mabao mawili kati ya hayo yakifungwa na Paul Pogba ambaye amehusika kwenye mabao sita kati ya 12 kwenye mechi tatu zilizopita akifunga manne na kutoa pasi za mabao mbili huku mabao mengine yakifungwa na Marcus Rashford na Romelu Lukaku.

Manchester United imeshinda michezo yote mitatu ikiwa chini ya Ole Gunnar Solskjaer na sasa wanashika nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England wakiwa alama tatu nyuma ya Arsenal wanaoshika nafasi ya tano.