Japan yafuta mchezo wake dhidi ya Chile

0
2205

Japan imefuta mchezo wake wa kirafiki dhidi ya Chile uliotakiwa kuchezwa Septemba Saba mwaka huu, kufuatia tetemeko la ardhi kukikumba kisiwa cha Hokkaido.

Mchezo huo wa kirafiki dhidi ya Chile ulitakuwa kuchezwa kwenye mji wa Sapporo Dome.

Chama Cha Soka cha Japan (JFA) kimesema kuwa kimefikiria kuhusu suala hilo na kuamua kuchukua maamuzi ya kuufuta mchezo huo.

Taarifa iliyotolewa na JFA imesema kuwa kutokana na tetemeko hilo la ardhi wameona ni vema kuufuta mchezo huo.

Rais wa JFA, -Tashima Kohzo amesema kuwa wote kwenye chama cha soka pamoja na wachezaji wamesikitishwa na tukio hilo na wapo pamoja na wakazi wa Hokkaido.

Mchezo dhidi ya Chile ungekuwa wa kwanza kwa kocha mpya wa timu ya Taifa ya Japan, – Hajime Moriyasu ambaye ameanza kuinoa timu hiyo mara baada ya kumalizika kwa michuano ya kombe la Dunia.

Japan pia imepanga kucheza mchezo mwingine dhidi ya Costa Rica Septemba kumi na moja mwaka huu kwenye mji wa Osaka.