Giresse kocha mpya Tunisia

0
1732

Shirikisho la soka nchini Tunisia limemteua nyota wa zamani wa timu ya Taifa ya Ufaransa, – Alain Giresse kuwa kocha mpya wa timu ya Taifa kuchukua nafasi ya Faouzi Benzarti.
Benzarti alitimuliwa kazi mwezi Oktoba mwaka huu, siku nne tu tangu alipokipeleka kikosi cha Taifa hilo katika fainali za mataifa ya Afrika za mwaka 2019 ambazo mpaka sasa bado haijajulikana zitafanyikia wapi.

Giresse anayechukua nafasi ya Benzarti ataanza rasmi kukinoa kikosi cha Tunisia Januari Mosi mwaka 2019 huku mkataba wake ukitarajiwa kufikia kikomo Juni 2020.
Kocha huyo mwenye umri wa miaka 66, ana uzoefu wa kutosha kwenye soka la Afrika ambapo amevinoa vikosi vya mataifa ya Gabon, Senegal na Mali ambayo ameifundisha mara mbili.

Mapema mwaka huu, kocha huyo pia alikuwa akihusishwa kwenda kukinoa kikosi cha timu ya Taifa ya Cameroon lakini nafasi hiyo ilichukuliwa na Clarence Seedorf akisaidiana na Patrick Cluivert.