Zanzibar kuendelea kushirikiana na wahisani

0
186

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Mwinyi amesema, serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wahisani katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Dkt. Mwinyi ameeleza hayo alipokutana na kufanya nazungumzo na Dkt.Charlotte Hawkins aliyefika Ikulu Zanzibar.

Amesema Zanzibar inahitaji wataalamu wengi zaidi kutoka nje, ili kusaidiana na wataalamu wazalendo hatika kuimarisha utoaji wa huduma za kijami ikiwa ni pamoja afya na elimu.

Rais Mwinyi amesema ujio wa Dkt. Hawkins nchini na kujikita katika kukabiliana na changamoto inayowakabili watoto wanaozaliwa na hitilafu katika miguu imewawezesha watoto wengi kunufaika na huduma zilizotolewa.

Kwa upande wake Dkt. Charlotte Hawkins ambaye ni bingwa wa upasuaji kutoka nchini Uingereza amemueleza Rais Mwinyi kuwa, amefurahia ushirikiano alioupata kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambao umemuwezesha kufanikisha majukumu yake.

Dkt. Charlotte Hawkins amekuwepo nchini kwa kipindi cha miaka 13 akisaidia juhudi za serikali katika kukabiliana na changamoto zinazowakbili watoto wachanga wanaozaliwa wakiwa na miguu yenye hitilafu.