Zabuni ya kutengeneza kivuko kipya kutangazwa

0
2297

Rais John Magufuli ameagiza kutangazwa kwa zabuni ya haraka ya kutengeneza kivuko kingine kipya chenye uwezo wa kubeba tani 50 za mizigo na abiria zaidi ya 200 kitakachotumiwa na Wakazi wa kisiwa cha Ukara wilayani Ukerewe mkoani Mwanza.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika kisiwa cha Ukara, ikiwa ni siku chache baada ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere.

“Hili ni agizo la Mheshimiwa Rais, na mimi ninamuagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe aitishe zabuni hiyo haraka sana, kazi hiyo ifanywe mara moja ili kivuko kipya kiweze kutengenezwa na kusaidia wananchi wa eneo hili kwa haraka,” amesema Waziri Mkuu Majaliwa.

Waziri Mkuu Majaliwa  amesema kuwa  kivuko hicho kipya kikikamilika, kitapangiwa ratiba za safari nyingi zaidi badala ya kwenda mara moja kwa siku ili kuondoka kero iliyokuwa ikiwakabili wakazi wa eneo hilo.