Waziri Mkuu Majaliwa awashukuru Wananchi Ruangwa kujenga uwanja

0
179

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Ruangwa mkoani Lindi, amewapongeza Wananchi wa Ruangwa kwa juhudi zao za kujitoa kuchangia ujenzi wa uwanja wa Majaliwa uliopo Ruangwa mkoani Lindi.

Akihutubia Wananchi waliojitokeza kwenye uzinduzi wa uwanja huo Waziri Mkuu amesema uwanja huo utakuwa na mchango mkubwa wa kukuza vipaji vya wananchi wa Lindi na mikoa ya kusini pamoja na maendeleo ya soka nchini.

Aidha Waziri Mkuu amesema mchakato wa wa Ujenzi wa uwanja huo ulijumuisha wananchi wote bila kujali itikadi za vyama huku akiwapongeza umoja wa Vijana CCM-Ruangwa kwa kufyatua tofali elfu sitini zilizotumika kujenga ukuta wa uwanja huo.

“Niwashukuru sana UVCCM kwa kufyatua tofali elfu sitini za kujenga ukuta wa uwanja, niwashukuru Umoja wananwake CCM UWT kwa kumwagilia maji tofali hizo na Jumuiya ya Wazazi CCM kuzipanga. Lakini niwashukuru wananchi wote na wanasiasa wa vyama vingine walishiriki kubeba kusogeza eneo la Ujenzi wa uwanja” -ameongeza Waziri Mkuu.

Uwanja wa Majaliwa Ruangwa umekamilika katika eneo la kucheza mpira na kufunga taa za kisasa huku Ujenzi wa maeneo mengine ikiwemo maeneo ya utawala na kuzungusha ukuta ukiendelea.