Waziri aagiza wanaozusha taarifa za vifo washughulikiwe

0
316

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza vyombo husika kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaosambaza taarifa za uongo mitandaoni kuhusu afya za watu wengine.

Dkt. Nchemba amesema hayo kufuatia uwepo wa uvumi mwingi mitandaoni kuhusu hali za afya za watu mbalimbali huku akifafanua kwamba, kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Mitandao kinazuia watu kutoa taarifa za uongo.

“Kumetokea tabia mbaya ya kuzushiana, (na fulani anaumwa, na fulani naye anaumwa. Mara nasikia fulani amekufa na fulani naye amekufa). Huku ni kukosa utu, ni kuathiri maisha binafsi ya mtu, familia yake na kusababisha taharuki kwenye Jamii.

“Nimeelekeza vyombo vyote husika kuchukua hatua bila kusubiri mtu binafsi akalalamike,” amesema waziri huyo.

Aidha, amewataka wananchi kuacha tabia hiyo mara moja.

Tanzania inaendelea na maombolezo kufuatia vifo vya aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Seif Sharif Hamad na aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi.