Wauguzi wapongezwa kwa kazi nzuri

0
132

Katika kuadhimisha siku ya Wauguzi duniani hii leo. baadhi ya Wakazi wa mkoa wa Arusha wametoa maoni yao kuhusu huduma zinazotolewa na Wauguzi pindi wanapohitaji huduma kutoka kwao.

Wamemweleza mwandishi wa TBC kuwa, Wauguzi wamekuwa wakiwahudumia vizuri, japo kuna changamoto kadhaa zinazoweza kutatuliwa ili kuleta tija katika kada hiyo.

Mmoja wa Wakazi hao ni Doreen Silayo ambaye amekiri kuwa kazi ya uuguzi ni ngumu. lakini mara zote alipokwenda hospitalini amekuwa akihudumiwa vizuri, huku Varelia Msaki akitoa wito kwa Wauguzi ambao hawatimizi wajibu wao kutumia maadhimisho ya siku ya Wauguzi Duniani kama chachu ya kuwakumbusha kutoa huduma bora kwa wagonjwa.

Wakati maadhimisho ya siku ya Wauguzi Duniani yakiendelea, baadhi ya maofisa ustawi wa jamii, wahudumu wa afya pamoja na azaki zianazotoa huduma za afya ya jamii mkoani Arusha wanaopatiwa mafunzo wamesema, kunahitajika elimu zaidi ya uelewa wa masuala ya afya ya akili na saiokolojia.

John Ambrose ambaye ni Mkurugenzi wa taasisi ya PHEDES Tanzania iliyoandaa mafunzo hayo amesema, siku ya Wauguzi duniani inawakumbusha Wauguzi hao kuzingatia weledi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.