Watu watatu wanashikiliwa polisi kwa tuhuma za ujangili

0
895

Jeshi la Polisi Mkoani Iringa linawashikilia watu watatu kwa tuhuma za kuhusika katika matukio ya ujangili wa tembo katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha Mkoani Iringa.

Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Juma Bwire amesema watuhumiwa hao wamekamatwa kufuatia taarifa za wasamaria wema ambapo wamekutwa na bunduki mbili aina ya gobore zinazosadikiwa kutumika kwenye uwindaji huo haramu.

Kukamatwa kwa watuhumiwa watatu wa ujangili kumekuja siku chache baada ya kuripotiwa kurejea tena kwa kasi vitendo vya ujangili wa tembo katika Hifadhi ya Ruaha ambavyo vilikuwa vimepungua kwa kiasi kikubwa.

Katika kipindi cha mwaka jana inakadiriwa kuwa tembo sita walikutwa wameuawa kwenye eneo la nje ya Hifadhi ya Ruaha hali iliyoashiria kuwa wawindaji haramu wameanza tena ujangili wa tembo.

Katika hatua nyingine, Jeshi la Polisi Mkoani Iringa limewatia mabaroni watuhumiwa watano akiwemo dereva wa lori la kusafirisha mafuta kwa wizi wa Lita Elfu 38 za mafuta ya Dizeli yaliyokuwa yanasafirishwa kwenda nchini Zambia.