Watoto kupata chanjo dhidi ya Malaria

0
218

Watoto Barani Afrika wanatarajiwa kuanza kupatiwa chanjo dhidi ya ugonjwa wa malaria, ikiwa ni jitihada za kupambana na ugonjwa huo.
 
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Tedros Ghebreyesus amesema chanjo hiyo itaanza kutolewa baada ya kupatikana kwake, ikiwa ni hatua ya mafanikio makubwa katika sekta ya afya.

Amesema kupatikana kwa chanjo hiyo ya malaria kwa watoto iliyokuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu, ni mafanikio makubwa katika sayansi, afya ya watoto pamoja na udhibiti wa malaria.

Chanjo hiyo ya malaria kwa watoto inatarajiwa kuokoa maisha ya maelfu ya Watoto kila mwaka Barani Afrika.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa WHO anayesimamia mpango wa malaria Dkt. Pedro Alonso amesema kupatikana kwa chanjo dhidi ya malaria ni mafanikio makubwa kisayansi kwa kuwa chanjo hiyo imekuwa ikitafutwa kwa zaidi ya miaka 100,  na inatarajiwa kuokoa maisha na kuzuia ugonjwa huo kuenea kwa Watoto Barani Afrika.