Watanzania watakiwa Kujitegemea wenyewe kiuchumi

0
1172

Rais John Magufuli amesema watanzania wanatakiwa kuitekeleza dhana ya kujitegemea kwa ajili ya maendeleo ya taifa lao.

Rais Magufuli ameyaema hayo Jijini Dar es salaam wakati akiongoza watanzania katika kupokea ndege mpya aina ya Airbus iliyonunuliwa na serikali kutoka nchini Canada ambapo amesema pasipo kujitegemea taifa halitaweza kupata maendeleo ya kujivunia.

Ndege mpya aina ya Airbus ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es salaam iliyonunuliwa na Serikali ya Tanzania kutokea nchini Canada.

Ndege hii Airbus 220-300 inafanya idadi ya ndege mpya zilizonunuliwa na serikali ya awamu ya tano mpaka sasa kufikia ndege sita.

Akihutubia wageni waliofika kushuhudia mapokezi ya ndege hiyo, Rais John Magufuli amewasisitiza watanzania kundelea kulipa kodi na kuishi katika dhana ya kujitegemea.

Rais Magufuli akatoa agizo kwa Shirika la Ndege nchini -Atcl kuanza kutumia ndege mbili zilizokuwa zikitumia na Rais kwa ajili ya kusafirisha abiria.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewahakikishia watanzania kuwa serikali itatekeleza ahadi zote walizoahidi wakati wa kuomba ridhaa ya kuliongoza taifa.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Atcl Mhandisi  Ladislaus Matindi amesema lengo la shirika hilo ni kuendelea kutoa huduma bora ya usafiri wa anga.

Ujio wa ndege mpya ya Airbus 220-300 iliyopewa jina la Ngorongoro inafungua wigo kwa Tanzania kuanza safari za ndege kwa nchi za nje ikiwemo Afrika Kusini, Zambia, India na China.