Watanzania watakiwa kuendelea kumshukuru Mungu

0
146

Watanzania wametakiwa kuendelea kumshukuru Mungu kutokana na maambukizi ya virusi vya corona kupungua kwa kiwango kikubwa tofauti na makisio yaliyotolewa awali na Shirika la Afya Duniani (WHO).

Akizungumza katika Ibada ya Jumapili, Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Kijitonyama jijini Dar es salaam, Dkt Eliona Kimaro amesema Tanzania imejaliwa kuwa na kiongozi imara mwenye maono makubwa tofauti na viongozi wa mataifa hata yenye nguvu kubwa za kiuchumi na kiteknolojia.

Dkt Kimaro amesema hatua ya Rais John Magufuli kuitisha maombi ya shukrani ni hekima ya kipekee kwa kiongozi wa nchi, huku akiwaonya wanasiasa kuacha kutumia corona kutafuta umaarufu wa kisiasa.

Alhamisi iliyopita Rais Magufuli aliwataka Watanzania wote kutumia siku tatu kufanya maombi ya shukrani kwa Mwenyezi Mungu baada ya maambuzi ya corona kuendelea kupungua kwa kasi.