Wasichana wenye miaka 10-24 waongoza kwa kutumia P2

0
359

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI imebaini ongezeko la matumizi ya vidonge vya kuzuia mimba miongoni mwa wasichana hasa wenye umri kati ya miaka 10 – 24.

Kamati imeeleza kuwa licha ya kuwa na lengo la kuzuia mimba, matumizi ya vidonge hivi ambavyo vimekuwa vikiuzwa kwa bei ya chini yamekuwa yakichochea maambukizi
ya Virusi vya UKIMWI.

Maambukizi hayo yanatokana na ukweli kwamba, baadhi ya wasichana wamekuwa wakiogopa zaidi mimba kuliko maambukizi ya VVU na hivyo wamekuwa wakitumia vidonge vya P2 kama njia mbadala ya kuzuia mimba na kuacha kutumia kondomu ambazo zingewakinga dhidi ya maambukizi ya VVU, magonjwa ya ngono na mimba zisizotarajiwa.

Ili kukabiliana na tabia hiyo hatarishi, kamati imeshauri kwamba, wakati wa mauzo ya dawa za kuzuia mimba (P2) ni vizuri zikauzwa pamoja na kondomu kwa lazima ili kuwawezesha wasichana kuwa na tabia ya kutumia kondomu hizo bila ya kunyanyapaliwa.