Wanaovuta sigara hadharani kuchukuliwa hatua

0
220

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), imesema itawachukulia hatua za kisheria watu watakaobainika kutumia bidhaa za tumbaku hadharani hasa sigara kutokana na madhara yanayotokea.

Kaimu Meneja TMDA Kanda ya Mashariki, Gloria Matemu amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati akitoa elimu katika kituo cha mabasi
yaendayo haraka eneo la Gerezani.

Matemu amesema Sheria ya udhibiti wa tumbaku sura ya 121 inakataza kwa watumiaji bidhaa za tumbaku, kuvuta sigara hadharani, ambapo adhabu ni faini shilingi 200,000 au kifungo cha miezi sita jela.

Pia alieleza kuwa sheria hiyo inataka wamiliki wa maeneo ya umma, kutenga sehemu maalum kwa ajili ya kuvutia bidhaa za tumbaku na kuweka alama maalum kwa ajili ya shughuli hiyo.

Ameongeza kuwa sheria inakataza kutoa matangazo au kudhamini matangazo kwa kupitia vyombo vya habari, vipeperushi au sauti zilizorekodiwa.