Wanaojihusisha na magendo Karagwe waonywa

0
1799

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini Simon Sirro amesema kuwa jeshi hilo linaendelea na uchunguzi dhidi ya raia na askari wa jeshi hilo wanaotuhumiwa kujihusisha na biashara ya magendo ya kahawa kwenda nchi jirani.

IGP Sirro ametoa kauli hiyo wakati wa ziara yake wilayani Karagwe mkoani Kagera.

Kufuatia kuendelea kwa biashara ya magendo ya kahawa mkoani Kagera, IGP Sirro amewataka watu wote wanaojihusisha na biashara hiyo kuacha mara moja kabla operesheni maalum ya kupambana na magendo haijawafikia.

Akiwa wilayani Karagwe, Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi nchini pamoja na mambo mengine, ameweka jiwe na msingi la ujenzi wa jengo la idara ya upelelezi na lile la ujenzi wa idara ya usalama barabarani.

Ujenzi huo unasimamiwa na Jeshi la Polisi nchini kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani Karagwe, ambapo IGP Sirro ameahidi kuchangia shilingi milioni Tano ili kukamilisha ujenzi huo.