Wamachinga wapewa mikopo ya gharama nafuu

0
379

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa ametoa wito kwa sekta za kifedha na taasisi binafsi kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kutoa huduma za mikopo ya gharama nafuu kwa ajili ya kukuza biashara za wajasiriamali wadogo.

Akifungua kongamano la Jukwaa la Maendeleo ya Sekta ya Fedha leo tarehe 20 Mei, 2022, Jijini Dodoma, Bashungwa ameziomba taasisi  kuinua kundi hilo kwa lengo  kwa kutoa mikopo ili kuboresha mazingira ya biashara na kuinua wigo wa ulipaji kodi.

Bashungwa amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan  kwa dhamira ya kutambua Wamachinga  kuwa sekta rasmi na kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya biashara.

Amewahakikishia wajasiriamali wadogo wote nchini kuwa Serikali ina dhamira ya dhati katika kuhakikisha inatengeneza mazingira wezeshi kwa ajili yao, hivyo wizara husika  zitahakikisha zinatekeleza kwa weledi dhamira ya Rais Samia ya kuleta maisha bora kwa machinga inafanikiwa.

Aidha, amewaagiza Makatibu wa  Wizara ya fedha, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, jinsi, wazee na mahitaji Maalum  na Ofisi ya Rais TAMISEMI  kukaa kwa pamoja ili kujadili na kuchambua maazimio ya kongamano hilo na kupata muelekeo wa Sekta ya Machinga nchini