Waliohusika kukeketa Mabinti Wasakwe

0
310

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Meja Jenerali Suleiman Mzee ameagiza kukamatwa kwa wazazi na walezi 70 waliohusika kukeketa watoto waliorejea majumbani kutoka katika hifadhi ya nyumba salama baada ya kukimbia ukeketaji.

Mzee ametoa agizo hilo baada ya kupokea taarifa ya kuwepo kwa idadi hiyo ya watoto waliokeketwa, na kuvitaka vituo hivyo kutowaruhusu kurejea makwao watoto waliosalia.

Ameitaka kamati ya ulinzi na usalama kuhakikisha inaharakisha oparesheni hiyo ili wahusika wachukuliwe hatua haraka iwezekanavyo.

Ameelekeza pia kukamatwa kwa wazee wa mila pamoja na viongozi wa serikali za vijiji na mitaa huku akisema kuendeleza vitendo hivyo ni kupingana na Serikali kwenye mapambano dhidi ya kupinga ukatili mkoani humo.