Wachezaji wa zamani na matamanio ya kuendeleza soka

0
107

Wachezaji wa soka wa zamani hapa nchini wamesema kuna umuhimu kwao kuwa na jukwaa maalumu la kutoa elimu kuhusu mchezo wa soka ili uwe na tija kwa Taifa.

Wameyasema hayo walipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Dkt. Ayub Rioba Chacha katika ofisi za TBC Mikocheni, Dar es Salaam, mazungumzo yaliyokuwa na lengo la kujadili namna ya kuendeleza mchezo wa soka hapa nchini.

Aidha wachezaji hao wa soka wa zamani wameomba kuwepo kwa mfumo maalumu ambao utawatambua kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kulitumikia Taifa kupitia mchezo wa soka.

Kwa upande wake Dkt. Ayub Rioba Chacha amesema TBC inatambua mchango mkubwa wa wachezaji hao wastaafu wa soka na itashirikiana nao katika kuanzisha jukwaa maalumu ili kuzungumzia na kutoa elimu kuhusu maendeleo ya soka nchini.

Baadhi ya wachezaji hao ni Faza Lusozi, Carlos Mwinyimkuu, Jamal Rwambo, Mhandisi Alhaji Fereshi, Abas Kuka, Sunday Manara, Rahim Lumerez na Athanas Maiko ambao wamecheza katika vilabu vya ndani na nje ya Tanzania pamoja na timu ya Taifa.

TBCOnlineUpdates