Vyama vya siasa vyaagizwa kufungua ofisi jijini Dodoma

0
491
Msajili Msaidizi wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza.

Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imetoa wito kwa vyama vya siasa kufungua ofisi za makao makuu jijini Dodoma kwa kuwa ndiyo makao makuu ya serikali, na ndipo shughuli zote za serikali zinapofanyka.

Wito huo umetolea na Msajili Msaidizi wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza, alipotembelea ofisi ndogo za makao makuu ya Chama cha Wakulima (AAFP) jijini Dodoma hivi karibuni.

“Natoa wito kwa vyama vingine vya siasa ambavyo havina ofisi ndogo za makao makuu jijini Dodoma kufungua ofisi zao ukizingatia kuna vyama vya siasa ambavyo vinapata ruzuku ya Serikali ninategemea viwe na ofisi bora na nzuri hapa Dodoma kwa sababu uwezo huo wanao,

“Kama ambavyo mlienda kufungua ofisi za vyama vya siasa jijini Dar es Salaam kutokana na kuwa karibu na ofisi za serikali, natoa wito wa kufungua ofisi zao kwa kuwa huku ndiko makao makuu ya nchi na Serikali,” amesisitiza Nyahoza.

Ziara ya kutembelea ofisi ndogo za makao makuu ya vyama vya siasa jijini Dodoma ni muendelezo wa zoezi wa uhakiki wa vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu lililoanza Machi 17, 2020.

Katika ziara hiyo vyama viliyotembelewa jijini Dodoma ni pamoja na CCM, AAFP, NRA, CHADEMA, Demokrasia Makini na UMD.