Vijiji vyote kupata umeme

0
161

Serikali imesisitiza azma yake ya kupeleka nishati ya umeme katika vijiji vyote nchini.

Akijibu maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu Bungeni jijini Dodoma, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema utaratibu wa kupeleka umeme huo umegawanyika katika awamu tatu.

Ameliambia Bunge kuwa, awamu iliyopo sasa ya kupeleka nishati ya umeme vijijini ni ya pili ambapo Wakandarasi wamekwishasambazwa katika halmashauri zote nchini.

Waziri Mkuu Majaliwa ameongeza kuwa mkakati wa Serikali wa kupeleka nishati ya umeme maeneo ya vijijini umefanikiwa kwa kiasi kikubwa, kwa kuwa ni maeneo machache tu ndio yaliyobaki ambayo hayajapata huduma hiyo.

Pia ametoa wito kwa taasisi za kijamii ambazo zimepewa msamaha wa kodi katika uingizaji wa bidhaa, kuweka wazi ni bidhaa zipi wanazoziombea msamaha ili kuepuka urasimu katika uingizaji wa bidhaa hizo.