Utalii Mlima Kilimanjaro waendelea kama kawaida

0
267

Wizara ya Maliasili na Utalii imewatoa hofu watalii wanaotarajia kuja na waliopo nchini wenye lengo la kutembelea Mlima Kilimanjaro kuwa ajali ya moto uliozuka hivi karibuni haujaathiri shughuli za utalii.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangala amesema moto huo umethibitiwa.

“Moto uliowaka katika hifadhi ya mlima umedhibitiwa na hakuna wanyama walioripotiwa kuathirika kutokana na moto huo,” amesema Dkt. Kigwangala

Aidha Dkt.Kigwangala ameongeza kuwa licha ya kuwepo changamoto katika kuuzima moto huo shughuli za utalii zinaendelea kama kawaida.

Kwa upande wake afisa Mawasiliano huduma za misitu TFS Matha Chasama amewataka wananchi wanozunguka eneo la hifadhi ya mlima kuzingatia taratibu zinazofaa wakati wa kuandaa mashamba yao kwa ajili shughuli za kilimo ili kuepuka milipuko ya moto katika hifadhi.

Takribani watu 500 wakishirikiana na wataalamu wa TANAPA wamehusika kuongeza nguvu ya kuuzima moto huo uliozuka siku kadhaa zilizopita.