Ujenzi nyumba ya mkuu wa polisi wapigwa tafu

0
270

Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro limekabidhiwa mifuko 200 ya saruji, kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Rombo yenye thamani ya shilingi milioni tatu iliyotolewa na kiwanda cha saruji Moshi.

Akizungumza wakati akipokea saruji hiyo, Mkuu wa Operesheni wa Jeshi la Polisi mkoa wa Kilimanjaro Kamishna msaidizi wa Polisi Asterico Maiga amesema, saruji hiyo itasaidia kakamilisha kwa haraka ujenzi wa nyumba hiyo.

 ‘’Tunawaomba waendelee kulisaidia jeshi la polisi pale wanapoona inafaa kufanya hivyo, ili kudumisha mahusiano katika utendaji kazi wa kila siku.” Amesema Kamishna Msaidizi Maiga

Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro pia limetoa hati ya kutambua mchango unaotolewa na kiwanda hicho cha Saruji Moshi katika kulisaidia jeshi hilo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kiwanda cha Saruji Moshi, Tian Haifeng amesema wametoa msaada huo ikiwa ni moja ya mikakati ya kuunga mkono jitihada za Serikali za kumaliza changamoto ya nyumba za polisi.

Ujenzi wa nyumba hiyo ya Mkuu wa polisi wa wilaya ya Rombo, unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 81.4 hadi kukamilika kwake.