TOZO ZA HALMASHAURI KIKWAZO KWA BANDARI KAVU DSM

0
208

Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Mrisho Mrisho ameiomba Serikali kuingilia kati changamoto inayotokana na kutoza ushuru wa maegesho ya magari katika maeneo yanayosimamiwa na bandari ya Dar es Salaam.

Mrisho ameyasema hayo mkoani Dar es Salaam, alipokuwa akilitambulisha kwa Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile eneo maalumu litakalojengwa mitambo ya kuhifadhia bidhaa za vyakula zinazoharibika kwa haraka.

Amesema kwa sasa changamoto kubwa inayowakabili madereva wa malori katika bandari kavu za Dar es Salaam ni tozo hizo kutoka halmashauri huku akiitaja halmashauri ya Temeke kuwa ni mojawapo.

Amesema Bandari ya Dar es Salaam tayari inalipa ushuru wa huduma (Service Levy) kwa halmashauri, hivyo ingeendelea kutumia tozo hizo na kuwaacha madereva wa malori kupaki katika bandari hizo bila ya kuongezewa tozo zingine kwani kinachoendelea hivi sasa ni madereva hao kutafuta njia zingine za kukwepa tozo hiyo na kwenda kupaki malori barabarani.

Hivi sasa madereva wa malori wanaoegesha malori katika bandari Kavu Dar es Salaam wanatozwa na halmashauri gharama za kuegesha magari hayo, jambo walilodai kuwa ni kero kwao.