TBC yawashika mkono yatima

0
108

Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) limetoa msaada wa vitu mbalimbali ikiwa ni pamoja unga, mchele, mafuta na sukari kwa watoto wa kituo cha watoto yatima cha Yatima Trust Group kilichopo Chamazi mkoani Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vitu hivyo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa TBC Catherine Nchimbi ametoa wito kwa jamii kusaidia watoto yatima ili waweze kukua katika makuzi salama kama watoto wengine.

Mwanzilishi mwenza wa kituo hicho cha watoto yatima cha Yatima Trust Group
Winfrida Lubanzi ameishukuru TBC kwa msaada huo.

Amesema wana mahitaji mengi kwa ajili ya watoto wanaoishi katika kituo hicho hasa chakula na mahitaji ya shule.

Akisoma taarifa ya kituo, Mratibu wa kituo hicho Mrisho Sultan amesema, kituo hicho kimefanikiwa kutoa watoto 28 walio katika ajira mbalimbali na wengine wakiwa wamejiajiri.

Taasisi ya Yatima Trust ilianzishwa mwaka 1996 na hivi sasa kina jumla ya watoto 137.