TAKUKURU yakana kumhoji Mrisho Gambo

0
412

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Arusha imekanusha taarifa zinazosambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii na kwenye baadhi ya vyombo vya habari kwamba inamshikilia na kumhoji aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo.

Akitoa ufafanuzi Kaimu Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Arusha, James Ruge ameeleza kuwa taarifa zinazoeleza kuwa Gambo anashikiliwa na kuhojiwa kwa tuhuma za kutoa rushwa kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Mapinduzi mkoani Arusha si za kweli.

“Hatuwezi kufahamu wamezitoa wapi taarifa hizo lakini hazijatokea TAKUKURU mkoa wa Arusha,” ameeleza Ruge.

Aidha, taasisi hiyo mbali na kuwatahadharisha wananchi kujiepusha na usambazaji wa taarifa zinazozua taharuki, imewataka wanasiasa wenye nia ya kugombea katika uchaguzi mkuu mwaka huu kujiepusha na vitendo vya rushwa kwani wanawafuatiliwa kwa karibu.

“TAKUKURU nchi nzima inafuatilia nyendo za waliotangaza nia ya kugombea na wapambe wao kuhakikisha hawatoi rushwa kuchaguliwa katika ngazi yoyote.”