Serikali kuongeza vituo vya askari wanyamapori kukabiliana na tembo

0
169

Serikali  kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imeanza kujenga vituo vipya vya askari wa wanyamapori katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu hususan tembo.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, Francis Ndulane aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kudhibiti tembo wanaoharibu makazi na mashamba katika Kata za Kandawale na Miguruwe ambazo zinapakana na Pori la Akiba Selous.

“Kuna vituo 19 vya askari wanyamapori nchi nzima kwa mwaka huu wa fedha unaoishia lakini kuanzia Julai 1, 2022 Serikali itaongeza vituo 13 vya askari wanyamapori ili kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu,” Masanja amesisitiza.

Aidha, amesema Wizara imepata kibali cha kuajiri askari wapya 600 ambao watasambazwa kwenye maeneo hatarishi.

Masanja ameongeza kuwa Wizara itaendelea na zoezi la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu mbinu za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu ili wananchi waweze kujikinga na wanyamapori hao.

Katika hatua nyingine, ameelekeza askari wanyamapori wa nyanda za juu kusini kuweka kambi katika kata ya Mbati na Marumba zilizopo Tunduru Kusini ambako tembo wameweka kambi kwa muda mrefu ili wawarudishe hifadhini.