Salamu za rambirambi zaendelea kutolewa

0
2316

Viongozi mbalimbali wameendelea kutoa salamu za rambirambi kwa Rais John Magufuli kufuatia ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere iliyotokea Septemba 20 mwaka huu na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 220 katika kisiwa cha Ukara wilayani Ukerewe mkoani Mwanza.

Salamu hizo ni pamoja na kutoka kwa Rais Vladimir Putin wa Russia, Rais XI Jinping wa China, Rais Brahim Ghali wa Saharawi, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya, Rais Frank-Walter Steinmeier wa Ujerumani, Waziri Mkuu wa Israel, – Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa Sweden,- Stefan Lofven, Kaimu Balozi wa Marekani nchini Inmi Patterson na Ofisi ya Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini.

Katika salamu zake, Rais XI Jinping wa China ameelezea kushtushwa na taarifa za ajali hiyo na kutuma salamu za pole kwa waliofiwa na walionusurika katika ajali hiyo.

Nayo Ofisi ya Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini imetuma salamu za pole kwa Rais Magufuli, familia za waliofiwa na Watanzania wote kufuatia vifo vya watanzania na kuwatakia manusura nafuu ya haraka na kuipongeza serikali ya Tanzania kwa kuchukua hatua za haraka kushughulikia suala hilo.

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu kwa niaba ya serikali na wananchi wa taifa hilo ametuma salamu za pole kwa wafiwa na kusema kuwa sala na mawazo yao yapo pamoja na watanzania katika kipindi hiki kigumu.