Rais Trump awataka Wamarekani kuwa wamoja

0
381


 
Rais Donald Trump wa Marekani amekuwa Rais wa kwanza nchini humo kushtakiwa mara mbili akiwa madarakani, baada ya bunge la Congress la nchi hiyo hapo jana kupitisha tena muswada mwingine wa kuridhia mwanasiasa huyo kushtakiwa.

Bunge hilo la Congress limeridhia Trump kushtakiwa tena, kutokana na hotuba yake aliyoirudia tena ya kuwa na mashaka na matokeo ya uchaguzi licha ya bunge hilo kutoa maamuzi na ile ya kuhamasisha wafuasi wake kufanya ghasia huko Capitol hill.

Trump amewataka Wananchi wa Marekani kuwa wamoja, lakini hakuzungumzia chochote kuhusiana na hatua ya bunge kuridhia ashtakiwe.

Kumekuwa na hisia mbalimbali miongoni mwa Wananchi baada ya taarifa za Trump kushtakiwa tena, baadhi wakionesha hofu na wengine wakisema kuwa huenda hatua hiyo ikaligawa taifa la Marekani.

Baadhi ya wafuasi wa Trump hivi sasa hawataki kuonesha wazi ushabiki wao wakihofia kuharibu biashara zao na wateja kuwakimbia.

Wakati huo huo Polisi wameimarisha doria mjini Washington DC wakati wananchi wakisubiri kwa hamu kuapishwa kwa mshindi wa kiti cha Urais nchini humo Joe Biden.