Rais Magufuli ataka matumizi sahihi ya ofisi za umma

0
918

Rais John Magufuli amewataka watendaji serikalini kuacha kufanya ofisi za umma kama mali zao binafsi bali ziwe mali ya watanzania na kulitumikia taifa kwa ujumla.

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo Ikulu jijini Dar Es Salaam baada ya kuwaapisha viongozi aliowateua Januari 8 ambapo amesema siku za karibuni umezuka mtindo kwa watendaji wa serikali kufanya ofisi za umma kama za kwao na kuwataka kuacha mara moja tabia hiyo.

Amewataka watendaji kutumikia wananchi kwa haki na kufuata sheria za nchi kwa kufanya maamuzi yenye tija na si kumuonea mtu.

“Naomba watendaji wote msichukue  ofisi za umma kama mali zenu, bali ziwe mali kwa watanzania na mkafanye majukumu kwa ajili ya nchi”alisema Rais Magufuli.

Rais amewataka kufanya kazi kwa weledi na wasiogope kufanya maamuzi pale inapotakiwa lakini isiwe kwa ubinfasi.

Janauri 8 Rais Magufuli alifanya teuzi za viongozi mbalimbali huku akifanya mabadiliko madogo katika baraza la mawaziri, kuteua Makatibu wakuu, Naibu Katibu Wakuu, Balozi na Katibu Tawala.