Rais ampandisha cheo Jaji aliyeendesha kesi kwa Kiswahili

0
185

Rais Dkt. John Magufuli amemteua Zepharine Galeba kuwa Jaji wa Mahakama ya rufani.

Kabla ya uteuzi huo Galeba alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa imeeleza kuwa uteuzi huo umeanza Leo Februari 1, 2021, na ataapishwa kesho saa 4:00 asubuhi Ikulu Chamwino mkoani Dodoma.

Mapema akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Tanzania, Rais alieleza kufurahishwa na kitendo cha jaji huyo kuendesha kesi kwa lugha ya Kiswahili.

Rais alisema jaji huyo amedhihirisha uzalendo na kuwataka maafisa wengine wa mahakama kuiga mfano huo kwa kutumia lugha ya Kiswahili inayoeleweka zaidi na Watanzania.