Polisi wadhibiti vurugu Mwanza

0
210

Jeshi la polisi mkoani Mwanza linawashikilia watu wawili kwa mahojiano zaidi kwa madai ya kuhusika na vurugu zilizozuka jijini Mwanza majira ya asubuhi hii leo kati ya kundi la vijana wanaosadikiwa kuwa ni wamachinga na mgambo.

Vurugu hizo zilisababisha taharuki miongoni mwa wakazi wa jiji hilo la Mwanza.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa amewatoa hofu wananchi na wafanyabiashara wa jijini humo na kusema vurugu hizo zimedhibitiwa na ulinzi umeimarishwa katika maeneo yote ya jiji.

Wakati wa vurugu hizo wafanyabiashara jijini Mwanza hasa katika mitaa  ya Nyerere, Liberty na Lumumba walilazimika kufunga maduka yao kutokana na vurugu hizo wakihofia usalama wao kutokana na mapambano ya kurushiana  mawe kati ya kundi la vijana hao na mgambo.

Baadhi ya wafanyabiashara katika jiji hilo la Mwanza wamesema, chanzo cha vurugu hizo ni viongozi kutosuughulikia malalamiko yao
huku wengine wakiitaka serikali iwachukulie hatua wahusika kwa kuwa vurugu hizo zinaumiza hata wasio na hatia.