Onyango atundika daluga Uganda The Cranes

0
199

Mlinda mlango wa kimataifa wa Uganda, Denis Onyango ameliandikia barua Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini humo (FUFA) akitoa taarifa ya kustaafu kuichezea timu ya Taifa ya Uganda, The Cranes.

Onyango ameitumikia Uganda katika michezo 83 tangu alipocheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa dhidi ya Cape Verde mnamo Juni 2005.

Mlinda mlango huyo anaondoka huku Uganda ikiwa imeshindwa kufuzu kucheza mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) ya 2022 huko Cameroon.

“Imekuwa furaha kubwa kuiwakilisha nchi yangu na nitashukuru kila wakati uzoefu na maarifa ambayo nimepata wakati nikichezea The Cranes,” ameandika Onyango.

Onyango kwa sasa anachezea klabu ya soka ya Mamelodi Sundown ambayo imefuzu hatua ya robo fainali ya Klabu Bingwa Barani Afrika.