Ngorongoro Heroes kujipima ubavu na Uganda leo

0
236

Timu ya taifa ya vijana ya chini ya miaka 20 (Ngorongoro Heroes) inashuka dimbani leo kucheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa na Uganda, mchezo utakaopigwa katika uwanja wa Chamazi Complex, Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 jioni.

Mchezo huo ni moja ya maandalizi ya kikosi hicho kwa ajili ya michuano ya Mataifa ya Afrika kwa vijana wa chini ya miaka 20 itakayofanyika nchini Mauritania kuanzia Februari 14 hadi Machi 6, 2021.

Pia, mchezo huo utatumiwa na jopo la makocha wa Ngorongoro Heroes kutazama uimara wa kikosi chao kabla ya michuano hiyo ya Africa ambapo Ngorongoro Heroes imepangwa kwenye kundi C pamoja na Ghana, Gambia na Morocco.

Hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kushiriki michuano ya Afrika kwa vijana wa chini ya miaka 20. Katika michuano hiyo, washindi wawili wa juu watafuzu kushiriki kombe la Dunia kwa vijana.