Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza uchaguzi mdogo katika kata mbili utakaofanyika Januari 19 mwaka 2019, uchaguzi utakaofanyika pamoja na ule wa jimbo la Temeke mkoani Dar es salaam na kata 46 za Tanzania Bara uliotangazwa hapo awali.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es salaam, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mbarouk Salim Mbarouk amezitaja kata hizo kuwa ni Mwanahina iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Meatu mkoani Shinyanga na Kata ya Biturana katika halmashauri ya wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma.
Amesema kuwa fomu za uteuzi wa wagombea hao zitatolewa kati ya Disemba 21 na 27 mwaka huu na uteuzi wa wagombea utafanyika Disemba 27 mwaka huu, huku kampeni za uchaguzi huo mdogo wa udiwani zikipangwa kuanza Disemba 28 mwaka huu hadi Januari 18 mwaka 2019.
Jaji Mbarouk ametoa wito kwa vyama vya siasa nchini kuzingatia sheria, kanuni, maadili ya uchaguzi, taratibu, miongozo na maelekezo yanayotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi wakati wa kipindi chote cha uchaguzi huo mdogo wa udiwani.