Mradi wa bomba la mafuta ni wa kimataifa

0
349

Serikali imesema utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda mpaka Chongoleani mkoani Tanga, Tanzania unazingatia viwango vya kimataifa pamoja na haki za binadamu.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa kauli hiyo wakati akisoma hotuba ya kuahirisha Bunge jijini Dodoma na kusema kuwa, kila hatua ya utekelezaji wa mradi huo inazingatia utu, haki za binadamu na utunzaji wa mazingira.

Kuhusu wanaohamishwa kupisha mradi huo Waziri Mkuu amesema, jumla ya kaya 331 zimefanyiwa tathmini na kila aliyepisha mradi huo amepewa uhuru wa kuchagua ama kujengewa nyuma sehemu nyingine ama kuchukua fedha na kwenda kujenga anapotaka.

Waziri Mkuu ameitaka Jumuiya ya Kimataifa na wadau wa maendeleo kufahamu kuwa, mradi huo haukiuki haki za binadamu wala hauna madhara yoyote kimazingira na kila aliyepitiwa na mradi huo amepatiwa haki yake.

Katika mkutano wa 8 wa Bunge, jumla ya maswali ya msingi 153 na maswali ya nyongeza 467 yameulizwa na wabunge na kujibiwa na serikali.

Bunge limeahirishwa hadi Novemba Mosi mwaka huu.