Moshi: Diwani wa CHADEMA aweka wazi sababu za kuhamia CCM

0
295

Diwani wa Kata ya Uru Kusini wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro kwa tiketi ya CHADEMA, Mwanasheria Wilhad Kitaly amejiunga na CCM kwa madai ya kukosekana kwa usawa na haki ndani ya chama chake hasa katika kuwatumikia wananchi.

Akizungunza na TBC wakati wa kukabidhi barua ya kujivua udiwani kwa ukurugenzi wa halmashauri hiyo, Kitaly amesema licha ya kuwa eneo ambalo si sahihi lakini alijitaidi katika kuwaletea wananchi wake maendeleo hasa katika sekta ya maji, ujenzi wa kituo cha polisi.

Amesema baadhi ya madiwani wenzake wa CHADEMA wamekuwa wakipiga vita na kupinga maendeleo jambo ambalo lilimfanya kubaini madiwani hao sio wenzake na hawakumuhitaji katika chama hicho.

Akipokea barua hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Kastory Msigala amewaondoa hofu madiwani ambao wameondoka vyama hivyo kwa kuwahakikishia serikali ipo katika kuwalipa stahiki zao zote kulingana na muda waliotumikia.

Wakati huo huo diwani huyo amekabidhiwa kadi ya CCM na Katibu wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Jonathan Mabhiya ambapo amemtaka mwanachama huyo kufuata misingi ya chama kwa kutekeleza ilani ya chama na kutetea masilahi ya wananchi.