Milioni 183 kuhudumia timu za Taifa

0
117

Serikali imetenga shilingi milioni 183 kwa ajili ya kuhudumia timu za Taifa kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023, ili kuziwezesha timu hizo kuwa na maandalizi ya kutosha kabla ya kushiriki mashindano ya kimataifa.

Naibu waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Pauline Gekul ameliambia Bunge kuwa, fedha hizo zimeziwezesha timu hizo kuwa na maandalizi ya kutosha na kushindana katika mashindano mbalimbali ikiwa ni pamoja na mashindano ya timu za Taifa za wanawake.

Naibu waziri Gekul amesema serikali pia imetenga shilingi bilioni 10, kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya viwanja vya michezo katika mwaka huu wa fedha.

Ameongeza kuwa tangu serikali imeanza kutenga fedha kwa ajili ya timu za Taifa za wanawake, kumekuwa na mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na timu ya Taifa ya wanawake ya umri wa chini ya miaka 17 kufuzu fainali za Kombe la Dunia.