Fundi Mkuu wa MV Nyerere aokolewa akiwa hai

0
2163

Fundi Mkuu wa kivuko cha MV Nyerere ameokolewa akiwa hai wakati zoezi la uokoaji likiendelea katika kisiwa cha Ukara wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza.

Mwandishi wa TBC aliyeko kisiwani Ukara anaripoti kwamba Fundi huyo Augustino Charahani ni miongoni mwa wafanyakazi wanane wa kivuko cha MV Nyerere ambaye alikuwemo katika kivuko hicho wakati ajali ikitokea.

Fundi huyo alikuwa amejifungia katika chumba cha injini ya kivuko hicho tangu ajali ilipotokea Septemba 20 mwaka huu.

Kazi ya uokoaji inaendelea ambapo mapema leo miili ya watu 25 imeopolewa.

Kufuatia msiba huo kwa taifa kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom imetoa shilingi Milioni kumi kwa serikali ili zitumiwe na wafiwa kusaidia katika mazishi ya wapendwa wao.