Mhagama atoa maagizo NSSF na OSHA

0
189

Waziri wa Kazi, Ajira vLVijana, Bunge na Watu wenye Ulemavu, Jenista Mhagama ameagiza Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii NSSF na Wakala wa Usalama wa Wafanyakazi Kazini (OSHA) kwenda katika kiwanda cha kutengeneza nondo cha Fujini kutoa elimu ya usalama kazini na kumaliza utata wa michango yao kuhifadhiwa.

Amesema hayo mjini Mkuranga wakati alipotembelea kukagua na kujiridhisha uhakika wa usalama na mazingira ya wafanyakazi kazini baada ya kiwanda hicho kufungwa na kufunguliwa baada ya wafanyakazi wawili kufariki dunia kiwandani hapo wakiwa kazini.

Amesema mkoa wa Pwani ni eneo la kimkakati kwa viwanda hivyo hoja za taarifa mbalimbali kutoka kwa mbunge wa jimbo hilo ambaye ni Naibu Waziri Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega ni lazima zichukuliwe hatua za haraka ili kuhakikisha usalama wa wafanyakazi wakiwa kazini.

“Kero alizozieleza hapa mbunge wenu zote ni muhimu na Serikali italifanyia kazi kwa haraka sana, lengo la serikali ni kuwalinda wawekezaji lakini pia kuhakikisha usalama na maslahi ya wafanyakazi yanazingatiwa” amesisitiza Mhagama

Kwa upande wake Ulega amesema mkoa wa Pwani hasa Mkuranga ni eneo la viwanda vingi na vimezalisha ajira nyingi kwa Watanzania hivyo ataendelea kulinda haki za wawekezaji na wafanyakazi kwa maslahi ya Taifa na wananchi kwa ujumla.