Mazishi ya waliofariki kwenye ajali kugharamiwa na serikali

0
215

Kufuatia ajali ya barabarani iliyotokea wilayani Korogwe mkoani Tanga na kusababisha vifo vya watu 14, serikali imesema itagharamia mazishi ya watu wote waliofariki katika ajali hiyo.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Omary Mgumba katika Hospitali ya Wilaya ya Korogwe, Magunga, alipofika kuwajulia hali majeruhi.

Katika ajali hiyo iliyotokea katika eneo la Magira Gereza, Tarafa ya Mombo wilayani Korogwe, barabara ya Segera – Buiko, watu wengine 12 walijeruhiwa.

Kati ya watu 17 waliofariki dunia, 14 ni wanafamilia waliokuwa wakisafirisha mwili
wa Athanas Mrema (59) aliyefariki dunia Februari Mosi mwaka huu na ulikuwa ukipelekwa kuzikwa wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro.

Ajali hiyo imehusisha magari mawili ambayo ni Mitsubishi Fuso na basi dogo aina ya Coaster ambayo ndiyo ilikuwa imebeba mwili wa marehemu.