Mavunde: Tutafanya utafiti wa madini nchi nzima

0
192

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde amesema Rais Samia Suluhu Hassan amewapa maelekezo wizara hiyo kufanya utafiti wa madini nchi nzima ili kupata taarifa sahihi za upatikanaji wa rasilimali za madini kwa maeneo husika hapa nchini ili kuwarahisishia wachimbaji kufanya shughuli zao katika maeneo sahihi yenye madini.

“Mheshimiwa Rais amenipa maelekezo ya kwamba ni hakikishe tunaendelea na kufanya utafiti [wa madini] Ili wachimbaji wasichimbe madini kwa kubahatisha. Wananchi hawa wanapoteza mitaji yao na nguvu zao kwa sababu hawana taarifa ya madini wanayoyachimba kwa sababu hatujafanya utafiti wa mkubwa kuifikia nchi nzima kubaini rasilimali za madini zilizopo,” amesema.

Aidha, Mavunde ameongeza kuwa, mwaka 2004 ulifanyika utafiti wa madini kwa kurusha ndege kwenye maeneo ya Kahama, Biharamulo, Mpanda na Nachingwea, maeneo ambayo ni sawa na ekari milioni 7 tu kati ya ekari milioni 233 za nchi nzima.

Mavunde ameyasema hayo wakati wa ziara ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko wilayani Bukombe mkoani Geita.